WAKATI sehemu ya makaburi imekuwa ikiogopwa na watu wengi kutokana na
 ukweli kwamba ni makazi ya wafu, hali ni tofauti kwa mtoto wa kiume 
anayekadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka 8-9 ambaye jina lake 
halikuweza kufahamika, kuishi katika makaburi ya Kigilagila, Yombo 
jijini Dar es Salaam kwa zaidi ya mwezi mmoja. 
 
Taarifa zilizopatikana kutoka eneo la tukio na baadaye kufuatiliwa 
kwa karibu na waandishi wetu, zinasema mtoto huyo ambaye hafahamiki 
alikotokea, alionekana akishinda na kulala katika makaburi hayo kwa 
zaidi ya mwezi mzima uliopita, kabla ya kutoweka kuelekea sehemu 
isiyojulikana.
Lakini baada ya siku kadhaa za kutoweka kwake, majirani wanasema 
walimuona tena mtoto huyo akiendelea na maisha eneo hilo ndipo walitoa 
taarifa Kituo Kidogo cha Polisi Yombo kuwataarifu juu ya tukio hilo 
lisilo la kawaida.
 
Polisi walifika makaburini hapo na kumchukuwa kijana huyo lakini 
walipomuhoji hakuweza kuongea chochote, hali iliyowafanya askari hao 
kutojua cha kufanya.
Kutokana na hali hiyo, polisi wa Kigilagila walifanya mawasiliano na 
Kituo cha Buguruni kwa hatua zaidi, ikiwemo kubaini anakotoka na sababu 
za kuishi katika mazingira hayo.
Gazeti hili lilifika na kumkuta mtoto huyo akiwa katika Kituo cha 
Buguruni anakohifadhiwa  wakati ndugu au wazazi wakisubiriwa, kabla ya 
taratibu za kumkabidhi kwa Ustawi wa Jamii kuanza kuchukuliwa.
Aidha, vyanzo vyetu ndani ya kituo hicho vilisema kuna watu 
walijitokeza wakiwa wanatafuta mtoto wa namna hiyo, lakini baada ya 
kumuona, walisema hakuwa yeye.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Ilala, SACP Marietha Minangi 
alithibitisha  kuwepo kwa mtoto huyo na kwamba taratibu zinafanywa ili 
kulimaliza tatizo lake.
“Natoa wito kwa wananchi waliopotelewa na kijana mwenye umri huo, 
kufika katika Kituo cha Polisi Buguruni ili kuweza kumtambua mtoto 
huyo,” alisema Kamanda Minangi.
credit: vituko vya mtaa 






0 comments:
Post a Comment